KARIBUNI WAFUGAJI WENZANGU

HISTORIA YA KUKU (WAMETOKA WAPI?)

Kuku alitokana na jamii ya kuku-mwitu mwekundu wa Asia. Muda si muda, mwanadamu alitambua kwamba kuku anaweza kufugwa kwa urahisi. Inashangaza kwamba miaka 2,000 hivi iliyopita, Yesu Kristo alizungumzia jinsi kuku anavyokusanya vifaranga vyake na kuvilinda chini ya mabawa yake. (Mathayo 23:37; 26:34) Mfano huo unaonyesha kwamba kwa ujumla watu walimfahamu sana ndege huyo. Lakini kuku walianza kufugwa kwa wingi na mayai kutagwa kwa minajili ya biashara katika karne ya 19.
Leo nyama ya kuku inapendwa sana kuliko nyama ya ndege mwingine yeyote. Kuku hufugwa na mamilioni ya watu—hata wale wanaoishi mijini—kwa ajili ya chakula na biashara. Kwa kweli, ni wanyama wachache sana wa kufugwa wanaoweza kusitawi katika maeneo mbalimbali kama kuku. Nchi mbalimbali zimekuza kuku wa jamii fulani ambao wanaweza kukidhi mahitaji yao na kustahimili hali ya hewa ya sehemu hizo. Baadhi ya jamii hizo ni: kuku wa Australorp kutoka Australia; kuku ajulikanaye sana wa Leghorn, asili yake ni Mediterania lakini anapendwa sana nchini Marekani; kuku wa New Hampshire, kuku wa Plymouth Rock, kuku wa Rhode Island Red, na Wyandotte, kuku hao wanatoka Marekani; na Cornish, Orpington, na Sussex, wanatoka Uingereza.

Sayansi ya kisasa imefanya ufugaji wa kuku uwe mojawapo ya utendaji wenye faida sana katika kilimo. Nchini Marekani, wakulima hutumia mbinu bora za ulishaji na ufugaji. Wao pia hudhibiti magonjwa ya kuku kwa njia za kisayansi. Watu wengi hushutumu mbinu hizo za kisayansi za kuzalisha kuku wengi kuwa za ukatili. Lakini licha ya shutuma hiyo wakulima wangali wanabuni njia bora zaidi za kufuga ndege hao. Hivi sasa mtu mmoja tu anaweza kutunza kuku 25,000 hadi 50,000 akitumia mbinu za kisasa. Ndege hao huwa wamefikia uzani wa kutosha kuuzwa sokoni baada ya miezi mitatu tu.*

Chanzo cha Nyama

Waweza kuona nyama ya kuku ikiuzwa karibu kila mahali, iwe hotelini, mkahawani, au kwenye soko la nyama na vinywaji. Kwa kweli, mikahawa mingi ulimwenguni pote huuza hasa kuku. Jamii fulani hupika nyama ya kuku kunapokuwa na sherehe za pekee. Na katika baadhi ya nchi, kama vile India, mapishi mbalimbali ya kuvutia ya kuku yamebuniwa. Mapishi kama vile lal murgi, kuku aliyepikwa kwa pilipili-hoho; kurgi murgi, kuku aliyechanwa; na adrak murgi, kuku aliyepikwa kwa mchuzi wa tangawizi, huwa na ladha sana!

Mbona kuku wanapendwa sana? Kwanza, ni vyakula vichache tu vinavyoweza kutayarishwa kwa kutumia vikolezo mbalimbali. Wewe hupenda kuku aliyepikwaje? Je, unapenda kuku aliyekaangwa, aliyechomwa, aliyebanikwa, aliyepikwa kwa mvuke, au aliyechemshwa polepole? Ukitazama kitabu chochote cha mapishi huenda ukaona mapishi mengi sana ya kuku yanayokusudiwa kuboresha ladha ya kuku.
Kuku huuzwa kwa bei nafuu pia kwa sababu wanapatikana katika nchi nyingi. Wataalamu wa lishe hupendekeza nyama ya kuku, kwa sababu ina protini, vitamini, na madini ambayo ni muhimu kwa afya. Na bado, nyama ya kuku ina kalori chache, asidi-mafuta chache, na mafuta mengine.

Kulisha Nchi Zinazositawi

Bila shaka, nchi nyingine hazina bidhaa tele za kuku. Jambo hilo lapasa kufikiriwa kwa sababu ripoti ya tume maalumu ya Baraza la Sayansi ya Kilimo na Tekinolojia, ilisema hivi: “Idadi ya watu ulimwenguni inatarajiwa kuongezeka kufikia bilioni 7.7 mwaka wa 2020 . . . Hata hivyo, sehemu kubwa (asilimia 95) ya ongezeko hilo inatarajiwa kutukia katika nchi zinazositawi.” Taarifa hiyo inatisha zaidi unapofikiria kwamba tayari watu wapatao milioni 800 wana utapiamlo!

Hata hivyo, wataalamu wengi wanaona kwamba kuku wanaweza kutumiwa kulisha watu hao wenye njaa na wakulima wanaweza kupata riziki kwa kuuza kuku. Tatizo ni kwamba si rahisi kwa wakulima maskini kufuga kuku wengi sana. Jambo la kwanza ni kwamba katika nchi maskini kuku hufugwa hasa kwenye mashamba madogo vijijini, au katika vizimba vidogo. Na katika nchi hizo, kwa kawaida kuku hawatunzwi katika mazingira salama. Wakati wa mchana kuku huachiliwa ili wazurure-zurure ovyo na kutafuta chakula, kisha hurejea nyumbani usiku, nyakati nyingine wanalala mitini au katika vizimba vya mabati.

Si ajabu kwamba kuku wengi wanaotunzwa hivyo hufa—baadhi yao kutokana na ugonjwa hatari wa Newcastle na wengine huuawa na wanyama na wanadamu. Wakulima wengi hawana ujuzi wala uwezo wa kulisha kuku wao ifaavyo, hawawezi kuwatengenezea makao yafaayo, au kuwalinda na magonjwa. Ndiyo sababu miradi ya kuwaelimisha wakulima katika nchi zinazositawi imeanzishwa. Kwa mfano, Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo, hivi majuzi lilianzisha mradi wa miaka mitano wa “kuwasaidia wakazi maskini wa Afrika wanaoishi mashambani kupitia ufugaji wa kuku.”

Tungali twasubiri kuona matokeo ya jitihada hizo nzuri. Basi ni jambo lifaalo kwa wakazi wa nchi tajiri kutambua kwamba mlo wanaoona kuwa wa kawaida kwao kama vile kipande cha kuku yamkini ni mlo ghali sana kwa watu wengi duniani. Kwa watu hao, kula kuku ni kama ndoto tu.

                                                          WASILIANA NASI KWA;
             
                                                                        0745 101842
                                                              hwilliady@ymail.com
 

No comments:

Post a Comment